Jumanne, 2 Juni 2015

EL MERREIKH WAJIVUA KOMBE LA KAGAME, WASEMA HAWAWEZI KUJA KULITETEA DAR



MABINGWA watetezi wa mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), El Merreikh ya Khartoum, Sudan imesema haitashiriki kutetea ubingwa wake wa michuano itakayofanyika kuanzia Julai 11 hadi Agosti 2 mwaka huu hapa nchini imefahamika.
Akizungumza na MANDELA MBEGEZE BLOG kutoka Khartoum, Ofisa Habari wa El Merreikh, Babiker Osman, alisema kwamba timu hiyo imeamua kujitoa kwenye mashindano ya Kombe la Kagame ni kutaka kuwekeza nguvu zaidi kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo Wasudan hao wameingia hatua ya makundi..

Osman alisema kuwa wanasikitika kuacha nafasi ya kutetea ubingwa wao na kuongeza kwamba wanaamini waandaaji wa michuano hiyo, Shirikisho la Soka la Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) wataelewa sababu zao za kujitoa kwenye michuano hiyo na wako tayari kushiriki kwenye michuano ya mwakani endapo watapata nafasi.

"El Merreikh haitashiriki Kombe la Kagame mwaka huu, sababu kubwa ni kujiandaa na mechi za makundi za mashindano ya Ligi ya Mabingwa, zitakuja timu nyingine kutoka Sudan", alisema Osman.
Alizitaja timu nyingine zitakazokuja kushiriki michuano hiyo kutoka Sudan ni Al Hilal ya Omdurman na Khartoum National ya Khartoum.
Baadhi ya timu nyingine zinazotarajiwa kushiriki mashindano hayo mwaka huu ni pamoja na Azam, Yanga, Simba zote za jijini Dar es Salaam, Gor Mahia (Kenya), KMKM (Zanzibar) na APR ya Rwanda.

El Merreikh ilifanikiwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Kagame mwaka jana jijini Kigali, Rwanda kwa kuwafunga wenyeji APR bao 1-0 katika mchezo wa fainali uliofanyika kwenye Uwanja wa Amahoro mbele ya Mlezi wa Cecafa na Rais wa nchi hiyo, Paul Kagame.

Bingwa wa michuano hiyo inayofanyika kila mwaka hupata zawadi ya Dola za Marekani 30,000 wakati mshindi wa pili huondoka na Dola za Marekani 20,000 huku timu itakayomaliza ya tatu itajinyakulia Dola za Marekani 10,000.
Katika mashindano hayo mwaka jana Tanzania Bara iliwakilishwa na Azam baada ya Yanga iliyokuwa chini ya Mbrazil, Marcio Maximo ambayo ilipaswa kushiriki kujitoa.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni